Siku niliyopotea sokoni
Timothy Kabare
Catherine Groenewald

Mimi ninaishi katika kijiji cha Kakuma. Ni mahali pakavu penye miti ya miiba na joto jingi.

Kakuma, kuna mbuzi wengi.

Wenyeji wengi hupanda baiskeli. Sokoni kuna maduka machache madogo.

1

Asubuhi moja, mamangu aliniita akasema, "Etabo, leo umefika umri wa miaka sita nasi tutakupa zawadi."

Nilimwuliza kwa furaha, "Zawadi gani? Akajibu, "Utafuatana nasi kesho twende sokoni. Tutapanda basi."

Hiyo ingekuwa safari yangu ya kwanza kwenda soko kubwa.

2

Keshoye, tulikwenda kwenye kituo cha basi.

Nilisimama kati ya mama na shangazi. Nilijisikia mdogo sana nikiwa kati yao.

Nilikuwa nimevaa suruali mpya ya bluu na fulana nyekundu.

3

Basi lilikuwa limejaa kwa hivyo ilibidi mama anipakate.

Nililala njia nzima Kwa vile nilikuwa nimechoka sana kutokana na joto.

Sikuona chochote.

4

Jua lilikuwa limeanza kuchomoza tulipofika sokoni. Langoni, palikuwa na mama muuzaji wa nafaka. Pembeni, walikuwapo wanaume wawili waliokuwa wakiviandaa viazi vitamu. 

Upande wa pili, mama mmoja mfupi alishika helikopta ya rangi ya bluu iliyometameta. Nilipoina, niliita, "Mama, mama, tazama helikopta ile!"

5

Katikati ya soko, kulikuwa na kibanda kikubwa. Matunda aina nyingi yaliuzwa pale.

"Yanaitwaje matunda haya?" Nilimwuliza mama huku nikimwonyesha aina ambayo sikuwahi kuiona.

6

Niliendelea kuuliza, "Na haya je?" Mama akajibu, "Haya ni matofaa."

Kati ya matunda yote kibandani, nilipenda matofaa zaidi. Nilipotazama umbo na rangi yake, niliwazia utamu wake.

"Tafadhali, ninunulie tofaa moja," nilimsihi mama.

7

Pindi nilipopewa tofaa, niliuachilia mkono wa mama, nikalishika tunda kwa mikono miwili.

Nililitafuna polepole nikaonja utamu wake. Nilikuwa sijawahi kulionja tunda tamu kama tofaa.

8

Nilipomaliza kulila tofaa, niligeuka kuongea na mama, lakini hakuwepo! Nilimtafuta mahali tulipotoka, lakini sikumwona yeye wala shangazi.

Nikamwuliza mama muuzaji nafaka, lakini hakujua walipokuwa.

Nikaanza kulia.

9

Baadaye, mama mmoja alinishika mkono na kuniongoza walipokuwa watoto wengine.

Mzee mmoja mwenye ndevu aliniuliza, "Jina lako nani mwanangu?"

Huku nikilia, nilimjibu, "E-ta-bo."

10

Nilianza kujiuliza kama watoto pia huuzwa sokoni. Mara nikaacha kulia ili nione kama wanunuzi wa watoto walikuwepo chumbani mle.

Baada ya muda alikuja mama mmoja akamchagua mmojawapo wa watoto.

Nikawaza, "Mimi nikichaguliwa, sitarudi nyumbani tena?"

11

Kisha nilimsikia yule mwanamume mwenye ndevu akiuliza, "Etabo yuko wapi?"

Nililia zaidi nikisema, "Lakini mimi sitaki kwenda na wewe!"

Nikatoroka.

12

Walipolisikia jina langu likiitwa, mama na shangazi walikimbilia chumbani humo.

"Etabo, Etabo." Iliita sauti niliyoitambua kuwa ya mamangu.

13

Nilimkumbatia mamangu. Kisha shangazi akasema, "Etabo, tulikuwa tunakutafuta tukupe zawadi yako ya siku ya kuzaliwa."

Aliitoa helikpta iliyometameta ya rangi ya bluu kutoka kwenye mfuko mkubwa alioubeba. "Hii hapa zawadi yako!" akasema mama.

14
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Siku niliyopotea sokoni
Author - Timothy Kabare, Ursula Nafula
Translation - Pete Mhunzi
Illustration - Catherine Groenewald
Language - Kiswahili
Level - Longer paragraphs