Wakati basi kubwa la bluu lilipochelewa
Mecelin Kakoro
Mango Tree

Mara moja kwa siku, basi kubwa la bluu husimama katika kijiji cha akina Bobo kuwasafirisha watu hadi mjini. Bobo hajawahi kuliona basi kubwa kama hilo. Anayahesabu madirisha 9 ya abiria na moja la dereva. "Lazima kuna safu 9 za viti vya abiria, kila safu ikiwa na takriban viti 8," Bobo anawaza.

Ikiwa ni sawa namna Bobo anavyowaza, je, basi kubwa la bluu linaweza kuwabeba abiria wangapi?

1

Kesho, mamake Bobo atampeleka mjini kununua sare mpya ya shule. Mama huuza mayai dazeni moja kwa shilingi 120. Karibu kila juma, yeye hupata jumla ya shilingi 3600. Je, ni mayai dazeni ngapi anazohitaji kuuza ili aweze kupata shilingi 3600? Kwa majuma 4 yaliyopita, aliweka akiba nusu ya fedha zake ili amnunulie Bobo sare mpya.

Je, unaweza kufanya hesabu ya kiasi cha fedha alizoweka akiba kwa muda wa majuma 4?

2

Takriban miezi mitatu imepita tangu Bobo asafiri kwa basi. Ana hamu kubwa ya kutaka kusafiri tena!

Kesho itakuwa siku kubwa. Inapofika saa moja jioni, Bobo yuko kitandani, lakini hapati usingizi wowote. Hafikirii jambo jingine ila tu safari yake ya kwenda mjini. Ni saa tatu na nusu, lakini Bobo bado hajalala.

3

Kila asubuhi, mama humwamsha Bobo saa moja. Lakini leo, Bobo tayari yuko macho inapofika saa kumi na mbili, ingawa usiku uliopita, aliweza tu kulala ilipotimia saa tano.

Inapotimia saa moja, Bobo ameoga na kuvaa, tayari kuondoka. Je, Bobo alipata usingizi kwa saa ngapi usiku uliopita?

4

Saa moja kasororobo asubuhi, Bobo na mamake wanawasili kituoni. Lile basi kubwa la bluu linastahili kuwasili kituoni inapotimia saa mbili asubuhi.

Mamake Bobo anaitazama saa yake. Lile basi kubwa la bluu tayari limechelewa kwa dakika kumi na tano. "Lakini, kawaida, basi hili halichelewi. Sijui kuna shida gani?" mama anasema.

5

Muda mfupi baadaye, watu zaidi wanajiunga nao pale kituoni. Wao pia wanazitazama saa zao na kuuliza kwa nini basi limechelewa. "Sasa tayari zimetimia saa tatu. Nitachelewa kufika kazini!" mwanamume mmoja aliyevalia suti nyeusi, anasema.

Bobo na mamake ndio waliosubiri kwa muda mrefu zaidi. Bobo anaona kama amesubiri kwa saa nyingi. Lakini, si saa nyingi. Je, wamekuwa wakisubiri kwa muda gani?

6

Bobo ana wasiwasi. "Je, nitaipata sare yangu kweli?" anamwuliza mamake.

Bobo anahesabu kwamba safari ya kwenda mjini na kurudi itawachukua saa 4. Saa 1 kufika huko, saa 2 kununua na saa 1 kurudi nyumbani. "Kuna mpira wa soka saa nane ambao mimi na marafiki zangu tumepanga kucheza. Basi lisipofika kwa wakati, nitachelewa kujiunga na wenzangu kwa mchezo huo."

7

Bado wanasubiri. Bobo sasa analia. Watu wawili walio kwenye foleni, wanaondoka na kurudi nyumbani. Wengine wanaendelea kuzitazama saa zao.

"Hebu tuwe na subira. Nina hakika kwamba basi litakuja hivi karibuni," mamake Bobo anawaambia. "Ninataka kwenda nyumbani!" Bobo analia kwa sauti. Mamake anamtuliza, "Tusubiri kwa dakika kumi tu. Basi lisipokuwa hapa saa tatu na nusu, tutaenda nyumbani."

8

Halafu, wanasikia mngurumo wa basi barabarani. "Si niliwaambia," mamake Bobo anasema. "Sasa ni saa tatu na nusu kamili. Tutanunua kwa haraka. Basi likiondoka mjini kwa wakati, tutafika nyumbani kwa wakati ufaao nawe utacheza mpira wa soka ulivyopanga."

Bobo anafuta machozi. Anahisi uchungu miguuni. Amechoka. Hawezi kusubiri kuliabiri lile basi.

9

La kushangaza ni kwamba, basi hili sio lile kubwa la bluu. Bali ni basi ndogo nyekundu. Bobo anahesabu madirisha ya abiria 4 pekee kisha anasema, "Mama, basi hii ni ndogo sana kuliko lile la bluu. Halitakuwa na nafasi ya kutosha kuwabeba watu wote wanaokwenda mjini."

Je, unakubaliana na Bobo? Unaweza kukisia idadi ya abiria ambao basi hiyo ndogo itaweza kubeba?

10

Mamake Bobo anamtania, "Wasiwasi wako hauna msingi. Angalau sote tunaosubiri hapa kituoni, tutapata nafasi ya kuketi."

"Hebu tuabiri kwa haraka ili tupate viti vizuri. Tumekuwa tukisubiri kwa muda mrefu zaidi ya wote!"

11

Bobo na mamake wanaabiri basi. Nyuma yao kuna watu 9 zaidi wanaotaka kuabiri. "Je, kutakuwa na viti vya kututosha sote?" Bobo anauliza.

Anaona kwamba kuna safu 4 za viti basini, upande mmoja ukiwa na viti 2 na mwingine ukiwa na viti 2 pia. Je, kuna viti vingapi jumla? Je, watu wote walio kwenye foleni wataweza kuketi?

12

Bobo na mamake wanakalia viti 2 vilivyo mbele karibu na mlango. Wana nafasi kubwa mbele yao na pia wanaweza kutazama nje vizuri.

Bobo anahesabu watu 6 wapya wanaojiunga na wengine kwenye foleni. "Hao wanafanya jumla ya idadi ya abiria kuwa 17," anawaza. "Mama, kuna nafasi ya kila mtu," Bobo anamweleza mamake. "Ni mtu mmoja tu atakayelazimika kusimama."

Je, Bobo alihesabu sawa?

13

Basi sasa imejaa. Dereva anaifunga milango na kuanza safari. Kuna kelele nje. Bobo na abiria wengine wanatazama dirishani.

Watu zaidi wanakimbia wakitaka kuifikia basi. Wanapiga mayowe, "Subiri! Subiri! Tunahitaji usafiri." Lakini wamechelewa. Bobo na mamake wanawahurumia walioachwa nyuma.

14

Mamake Bobo anamwuliza dereva, "Mbona hukujia lile basi kubwa la bluu?" Dereva anajibu, "Liliharibika jana. Hii basi ndogo nyekundu pekee ndiyo iliyopatikana."

"Je, na wale watu wote tuliowaacha nyuma?" mamake Bobo anauliza. Dereva anasema, "Usiwe na wasiwasi. Nitakuwa na safari mbili leo."

Bobo anasikiliza wanavyozungumza. Mawazo yake yanajaa nambari.

15

Bobo anahesabu viti tena. "Basi hii inawabeba watu 20, 16 wakiwa wameketi na 4 wakiwa wamesimama." Anajiuliza, "Basi hii itaweza kwenda safari ngapi ili iwapeleke abiria 100 mjini? Na abiria 200 au 150, je?" Unaweza kulipata jawabu?

Bobo amefurahi. Hivi karibuni, ataipata sare mpya. Kisha, basi itawarudisha nyumbani kwa wakati ili acheze soka.

16
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Wakati basi kubwa la bluu lilipochelewa
Author - Mecelin Kakoro
Translation - Ursula Nafula
Illustration - Mango Tree
Language - Kiswahili
Level - Read aloud