Hapo zamani za kale, palikuwa na panya wawili.
Mmoja aliishi kichakani.
Panya yule mwingine aliishi nyumbani.
Panya aliyeishi nyumbani alimwambia aliyeishi kichakani, "Unakula na kulala vibaya. Sisi tunalala na kula vizuri."
"Njoo ututembelee siku moja ujionee." Panya aliyeishi nyumbani alisema. "Niko tayari kuja usiku wa leo." Panya aliyeishi kichakani alijibu.
Wakati huo, mwenye nyumba alikuwa amekasirika sana. Alisema, "Hawa panya wanaokula chakula changu wataona!"
Aliweka mtego wa sukari.
Panya wale wawili waliingia mle nyumbani kula vinono.
Walicheka, "Chuchuchichicheche!"
Walipoufikia mtego, panya aliyeishi nyumbani alisema, "Hebu nionje hii sukari. Leo utajua vitamu tunavyokula hapa."
Lakini hata kabla ya panya kuonja sukari, mtego uliteguka, pa! Panya alishikwa shingoni. Macho yake yalivimba kama mbilingani.
Panya aliyeishi kichakani alitazama tu kwa mshangao.
Alisema, "Rafiki yangu, ni vitamu gani ulivyokula vilivyoyafanya macho yako kuvimba?"
Lakini, panya aliyeishi nyumbani hakuweza kumjibu.
Panya aliyeishi kichakani aliondoka pale akisema, "Haa! Sitaweza kuvifurahia hivi vitamu anavyovisifu."
Heri nyumbani kwako kubaya kuliko kwa jirani kuzuri.