Paka na Panya
Merga Debelo

Hapo zamani za kale, paka na panya walikuwa marafiki. Walifanya kazi na kucheza pamoja.

Walioana na kuishi kwa furaha.

1

Siku moja, panya walisema kwa hofu, "Baadhi ya jamaa zetu wamepotea."

"Sijamwona mjomba kwa muda," mmoja alisema.
"Sijamwona shangazi," alisema mwingine.

"Dadangu hayuko," alisema wa tatu. "Kakangu yuko wapi?" aliuliza wa nne.

2

Panya mmoja mzee alitikisa kichwa chake kwa huzuni akasema, "Marafiki wapendwa, nina habari mbaya. Paka wanatula. Ni lazima tuwe waangalifu. Hivi karibuni watatula sisi sote."

3

Panya waliingiwa na woga mwingi. Panya wa kike waliwaambia watoto wao, "Msiende nje. Kuweni waangalifu paka wasije wakawashika."

4

Panya wote walikuwa waangalifu sasa.

Walikaa katika mashimo yao na wala hawakwenda nje.

5

Sasa paka walikuwa na wasiwasi pia. Walisema, "Je, panya wote wamekwenda wapi? Tunahisi njaa na hatuna chochote cha kula."

"Wamejificha," paka mkubwa alisema. "Tunawezaje kuwakamata?"

6

Paka mwingine alisema, "Tutawauliza tupange ndoa kati yao nasi. Sherehe ya harusi itawaleta panya pamoja. Nasi tutawashika wote wakati mmoja tuwale!"

"Hilo ni wazo zuri sana," paka walisema.

7

Basi, paka waliwatuma wazee wao kwenda kuwaona panya.

"Tungependa tuwe na ndoa kati ya mmoja wa binti zenu na mmoja wa wavulana wetu," paka wazee waliwaambia panya.

8

Panya walisema, "Hatuwaamini. Mnataka kutula tu."

Paka walijibu, "La! Sisi ni waaminifu na wenye mioyo safi. Tunataka tuwe marafiki. Hapo zamani wengine wetu waliwala, lakini hilo halifanyiki tena. Hatutawahi kuwala tena."

9

Panya walipowatazama paka, waliona kuwa wote walikuwa wakitabasamu. "Tumekubali ndoa ifanyike kati ya mmoja wa binti zetu na mmoja wa mvulana wenu," panya walisema.

10

Paka walienda nyumbani kwa furaha.

"Siku ya harusi itakuwa nzuri sana," walisema huku wakilamba midomo yao.

11

Siku ya harusi, panya walikuwa bado na wasiwasi mwingi. "Kaeni karibu na mashimo yenu," waliwaonya wanao.

"Tazameni, paka wanakuja. Iwapo watakuwa wazuri kwetu, tutakuwa wazuri kwao. Lakini wakijaribu kutula, tutakuwa tayari kutoroka."

12

Paka walitokezea barabarani wakiimba wimbo wa harusi.

13

"Je, unayasikia maneno ya wimbo huo wanaoimba?" Panya mzee alimwuliza panya mchanga.

"Ndiyo," panya mchanga alijibu. Wimbo ulisema, "Washikeni muwale wote! Washikeni muwale wote!"

14

"Basi ni lazima tuimbe pia," alisema panya mzee.

Akaanza kuimba, "Kimbieni panya, kimbieni! Kimbieni panya, kimbieni!"

Panya wote waliruka ndani ya mashimo yao wakajificha.

15

Paka waliwasili wakaulizana, "Je, yuko wapi Bi. Harusi?"

Panya mzee alichomoza kichwa chake kutoka shimoni akawajibu, "Tumepata funzo. Maadui zako wakijifanya kuwa marafiki, ni lazima uwe tayari kutoroka."

16
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Paka na Panya
Author - Merga Debelo, Elizabeth Laird
Translation - Susan Kavaya
Illustration -
Language - Kiswahili
Level - Longer paragraphs