Ujasiri wa Nangila
Violet Otieno

Wekesa alikuwa na donda mguuni.

Yeye na mkewe waliishi kijijini na wanao.

1

Binti yao, Nangila, na kaka zake watatu walifanya kazi zao vizuri.

2

Nangila aliwavutia watu wengi.

Wanaume waliotaka kumwoa walitakiwa kutimiza sharti kali lililowekwa na babake.

3

Aliyetaka kumwoa Nangila alilazimika kuileta dawa ya kienyeji kutoka ziwa lililokuwa karibu. Ziwa hilo lilijaa mizimu hatari.

Ile dawa ya kienyeji kutoka ziwani tu ndiyo ingeponya lile donda alilokuwa nalo babake Nangila.

4

Baadhi ya wanaume waliojaribu kuipata ile dawa, walirudi mikono mitupu.

Wengine hawakurejea kutoka ziwani kamwe.

5

Nangila alikuwa na hofu kaka zake pia waliposhindwa kwenda ziwani. Aliamua kwenda mwenyewe.

Mamake alimwambia, "Mwanangu, ikiwa wanaume wenye nguvu wameshindwa, wewe utafaulu?"

Lakini, Nangila hakubadili nia yake.

6

Njiani, Nangila alimsaidia bi kizee mmoja kubeba kuni.

Bi kizee alimshukuru akasema, "Nitakueleza utakavyofika kwenye lile ziwa la mizimu na namna utakavyofanya."

7

Nangila alipofika ufukoni mwa ziwa, aliiona familia ya mizimu ikinywa na kusherehekea.

Alisubiri na kutazama. Mmoja baada ya mwingine, mizimu ilipatwa na usingizi.

8

Mizimu yote ilipolala, Nangila alipiga mbizi ziwani. 

Aliipata ile dawa na kuiweka mkobani. Alipokuwa akiogelea kurudi ufukoni, mawimbi makubwa yalimzunguka.

9

Ufukoni, mizimu ilikuwa imeamka. Nangila aliimba wimbo aliofundishwa na bi kizee:

Mie binti Wekesa, nilikuja kwani wanaume waliogopa. Babangu ahitaji dawa kupona donda. Nd'o sababu nipo pahali hapa pa kutisha, kwani ninyi ni viongozi.

10

Sauti ya Nangila ilikuwa tamu sana hata mizimu ikamtaka aimbe zaidi.

Kuimba kwake kuliifanya ilale tena. Nangila alikimbia haraka akafika kijijini.

11

Baada ya kutibu donda la babake, baba aliweza kusimama tena.

Kijiji kizima kilisherehekea na kumshangilia Nangila.

12

MASWALI: 1. Mwanamume yeyote aliyetaka kumwoa Nangila alilazimika kutimiza sharti lipi la babake? 2. Nangila alikuwa na kaka wangapi? 3. Nangila alisaidiwa na nani alipokuwa njiani? Alimfundisha Nangila nini? 4. Alipofika ufukoni mwa ziwa, Nangila alisubiri nini? 5. Nangila alifanya nini ili atoroke mizimu aliporudi ufukoni? 6. Kwa maoni yako, unafikiri Nangila ataolewa baada ya kutimiza sharti la babake yeye mwenyewe? Kama ataolewa, ataolewa na mtu wa aina gani?

13
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Ujasiri wa Nangila
Author - Violet Otieno
Adaptation - Ursula Nafula
Illustration -
Language - Kiswahili
Level - Longer paragraphs