Bibi atusimulia hadithi
Mutai Chepkoech
Marleen Visser

Tulikusanyika kwa bibi kuzisikiliza hadithi zake. Usiku huo, tuliketi karibu na meko bibi alipotusimulia hadithi:

Sungura na Tembo walikuwa majirani na pia marafiki.

1

Sungura alipenda uyoga, lakini alikuwa mvivu sana. Alizoea kuiba uyoga wa Tembo.

Mwaka mmoja, Tembo alipanda ndizi na maboga. Kwa hivyo, Sungura hakupata uyoga.

2

Sungura alikosa chakula kwa siku nyingi akaamua kuiba ndizi za Tembo. Tembo aligundua kwamba ndizi zake zilikuwa zikiibwa.

Alimwambia Sungura, "Kuna mtu ananiibia."

3

Sungura aliuliza, "Anaweza kuwa nani anayekuibia?"

Tembo alianza kuimba, "Nitamshika mwizi! Aaa! Nitamshika mwizi! Ooo!"

Sungura alikuwa na wasiwasi sana.

4

Tembo alimwuliza Kima amchungie shamba lake.

Lakini, Sungura hakuiba siku hiyo. Hakuiba siku iliyofuata pia.

Kima alichoka kuchunga akarudi nyumbani.

5

Siku iliyofuata, Sungura alienda shambani kwa Tembo kuiba tena.

Tembo alipoenda kukagua mimea yake, Sungura alijificha katika matawi ya maboga.

6

Tembo aliyaona matawi yakitingika akaanza kuimba, "Nimemshika mwizi! Aaa! Nimemshika mwizi! Ooo!"

Tembo alitafuta kila mahali lakini hakumpata mwizi.

7

Siku moja, Sungura alipokuwa akila mazao ya Tembo shambani, Tembo aliwasili.

Sungura aliruka na kujificha ndani ya boga moja kubwa.

8

Tembo aliliona lile boga kubwa akasema, "Ooo! Hapa kuna boga kubwa. Litakuwa chakula changu cha mchana."

Alilimeza papo hapo!

9

Sungura alijaribu kuruka nje ya lile boga, lakini hakuweza.

Tembo alipohisi kitu kikiruka tumboni mwake, alijiuliza, "Hili ni boga aina gani linaloruka tumboni?"

10

Tembo alilitema nje lile boga. Kabla kulikagua, Sungura alijitosa nje akatoroka.

Tembo hakuwahi kumshika mwizi.

11

Bibi alisema, "Na huo ndio mwisho wa hadithi."

"Asante bibi," tulimjibu. Tuliweka vikombe vyetu vya maziwa. Tukaenda kulala tukiwaza juu ya hadithi hiyo ya bibi.

12
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Bibi atusimulia hadithi
Author - Mutai Chepkoech
Translation - Ursula Nafula
Illustration - Marleen Visser
Language - Kiswahili
Level - First paragraphs