Ujasiri wa Nangila
Violet Otieno

Wekesa alikuwa na donda mguuni. Yeye na mkewe waliishi kijijini na wanao.

1

Binti yao, Nangila, na kaka zake watatu walifanya kazi zao vizuri.

2

Nangila aliwavutia wengi. Mwanamme aliyependa kumwoa, alitakiwa kutimiza sharti kali lililowekwa na babake.

3

Sharti lilikuwa kuileta miti-shamba kutoka ziwa lililokuwa karibu. Dawa hiyo ingeponya donda alilokuwa nalo bababke Nangila. Ziwa hilo lilijaa mizimu hatari.

4

Baadhi ya wanaume waliojaribu kuipata ile miti-shamba, walirudi mikono mitupu. Wengine kamwe hawakurejea kutoka ziwani.

5

Nangila alikuwa na hofu kaka zake pia waliposhindwa kwenda ziwani. Aliamua kwenda mwenyewe. Mamake alimwambia, "Mwanangu, wanaume wameshindwa, utafaulu?"

6

Nangila alimsaidia bi kizee mmoja kubeba kuni. Bi kizee alimshukuru, akamwambia, "Nitakueleza jinsi utakavyofika kwenye ziwa la mizimu na namna utakavyofanya."

7

Nangila alipofika kwenye ufuo wa ziwa, aliiona familia ya mizimu ikinywa na kusherehekea. Alisubiri na kutazama. Moja baada ya nyingine, mizimu ilipatwa na usingizi.

8

Mizimu yote ilipolala, Nangila alipiga mbizi ziwani. Aliipata miti-shamba na kuiweka mkobani. Alipoogelea kurudi ufuoni, mawimbi makubwa yalimzunguka.

9

Alifika ufuoni mizimu ikiwa imeamka. Aliimba wimbo aliofunzwa na bi kizee:

Mie nilikuja kwa sababu wanaume waliogopa. Babangu ahitaji dawa. Ndiyo sababu nikaja hapa.

10

Sauti ya Nangila ilikuwa tamu sana hata mizimu ikamtaka aendelee kuimba. Mizimu ilipolala tena, Nangila alikimbia haraka kwenda kijijini.

11

Baada ya kutibu donda la babake, babake aliweza kusimama tena. Kijiji kizima kilisherehekea na kumpongeza Nangila.

12
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Ujasiri wa Nangila
Author - Violet Otieno
Translation - Ursula Nafula
Illustration -
Language - Kiswahili
Level - First sentences