Nyumba ya Kobe
Maya Fowler
Katrin Coetzer

Siku moja, Kobe alikuwa akitembea nyasini.

Alichunguza mbele na kukodolea nyasi macho akamwona Konokono.

1

"Unatafuta nini?" Konokono alimwuliza.

"Ninaitafuta nyumba yangu. Umeiona?"

2

Alijibu, "La, sijaiona, lakini nitakusaidia kuitafuta!"

Konokono alipanda juu ya gamba la Kobe.

Kobe alimbeba Konokono mgongoni mwake. Walitafuta, lakini hawakuiona.

3

Baada ya muda mfupi, walimwona Ndege. "Mnatafuta nini?" Ndege aliwauliza.

"Ninatafuta nyumba yangu. Umeiona?" Kobe alisema.

"La, sijaiona, lakini nitakusaidia kuitafuta!" Ndege akajibu.

4

Ndege aliyapapatua mabawa yake na kupaa. "Unakwenda kwa kasi sana." Kobe alilalamika.

Ndege akamwambia, "Samahani, wacha nami pia niruke juu ya gamba lako."

5

Kobe aliwabeba Konokono na Ndege juu ya gamba lake.

Walitafuta bila kuona ishara ya nyumba ya Kobe.

6

Walipoendelea, walimwona Bunzi. "Mnatafuta nini?" Bunzi aliwauliza.

"Ninatafuta nyumba yangu. Umeiona?" Kobe alijibu.

7

Bunzi alisema, "La, sijaiona, lakini nitakusaidia kuitafuta!"

Aliruka mgongoni mwa Kobe. Kobe aliwabeba Konokono, Ndege na Bunzi.

Walitafuta, lakini hawakuona nyumba yoyote.

8

Hatua chache, walikutana na Panya. Alikuwa akitengeneza shada zuri la maua. "Unatafuta nini?" Panya aliuliza.

"Natafuta nyumba yangu. Umeiona?" Kobe alisema.

9

Panya alijibu, "La, sijaiona, lakini nitakusaidia kuitafuta!" Aliruka mgongoni mwa Kobe. "Subiri, siwezi kuacha maua yangu."

Panya alijinyoosha, akayakusanya maua yake huku Kobe akimsubiri.

10

Kobe aliendelea kutembea akiwabeba Konokono, Ndege, Bunzi na Panya mgongoni mwake. Walitafuta, lakini hawakuipata nyumba ya Kobe.

Upepo uliyapeperusha maua ya Panya. Kobe alikuwa amechoka sana. Akasema, "Ninyi ni wazito."

11

Upepo uliongezeka. Anga likabadilika likawa jeusi. "Ah, iwapi nyumba yangu?" Kobe aliuliza. Punde, radi ilinguruma milimani na umeme ukaangaza.

Mara mvua ikaanza kunyesha. "Ah, iwapi nyumba ya Kobe?" Konokono, Ndege, Bunzi na Panya waliuliza.

12

Upepo ulizidi kuvuma na kuvuruga.

Ghafla, upepo uliwapeperusha wote kutoka mgongoni mwa Kobe.

13

Mvua ya mawe ikaanza kunyesha. Kwa uoga, Kobe alijikunja na kuingia ndani ya gamba lake.

Mle ndani mlikuwa joto. "Kumbe, hii ndiyo nyumba yangu!" Kobe aliwaza.

14

Konokono, Ndege, Bunzi na Panya walijikusanya chini ya gamba la Kobe.

Wakatambua, "Ah, hii ndiyo nyumba ya Kobe!"

15
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Nyumba ya Kobe
Author - Maya Fowler
Translation - Brigid Simiyu
Illustration - Katrin Coetzer
Language - Kiswahili
Level - Longer paragraphs