Mtoto Punda
Lindiwe Matshikiza
Meghan Judge

Siku moja, msichana mdogo aliona umbo la ajabu kwa umbali.

1

Umbo hilo lilipokaribia, aligundua kwamba lilikuwa mwanamke mja mzito.

2

Kwa ushupavu, msichana huyo alimkaribia yule mwanamke mja mzito.

Jamaa zake wakasema, "Hatuna budi kumkaribisha akae nasi. Tutamlinda hadi atakapomzaa mtoto wake."

3

Baadaye, mama huyo alikuwa tayari kujifungua.

Majirani wakashughulika. "Sukuma! Leta blanketi! Maji! Suukuumaaa!"

4

Mama alijifungua.

Majirani walipomwona mtoto, wote walirudi nyuma kwa mshtuko.

"Punda!"

5

Wakaanza kugombana. "Tulikubali kuwa tutamlinda huyu mama hadi atakapojifungua, na hivyo ndivyo tutakavyofanya," kiongozi wao alisema.

"Hapana! Tukifanya hivyo tutapata bahati mbaya!" alisema jirani mwingine.

6

Mama yule alijikuta peke yake tena.

Akajiuliza, "Nitafanyaje na mtoto huyu mwenye kunifedhehesha?"

7

Hatimaye, alikubali kuwa huyo ni mtoto wake na yeye ndiye mamake.

Mtoto punda angalibaki alivyozaliwa, mambo yangekuwa tofauti.

8

Lakini, alikua, akakua, hadi mamake akashindwa kumbeba mgongoni. Mamake mara nyingi alichoka na kuvunjika moyo.

Mara nyingine mtoto punda alimfanyisha kazi za kinyama.

9

Mtoto punda alikasirika akachanganyikiwa. Hangeweza kufanya lolote kama binadamu. Hakufanana na huyu wala yule.

Alizidi kukasirika hadi siku moja akampiga mamake teke akaanguka chini.

10

Mtoto punda aliona aibu.

Akakimbilia mbali kadiri alivyoweza.

11

Aliendelea kukimbia hadi usiku alipotambua kuwa amepotea.

"Hi ho?" Alinong'ona gizani. "Hi ho?" Mwangwi ukamrudia.

Alijikunja mahali akalala usingizi wa mang'amung'amu.

12

Kulipokucha, mtoto punda aliamka na kumkuta mzee wa ajabu akimtazama.

Naye pia akamtazama mzee machoni kwa hisia za matumaini.

Mzee akasema, "Njoo twende kwangu."

13

Mtoto punda alikubali mwaliko wa mzee huyo.

Mzee alimfundisha njia nyingi za maisha. Mtoto punda alijifunza mengi.

14

Asubuhi moja, mzee alimwomba mtoto punda ambebe hadi kilele cha mlima.

15

Walipofika juu mawinguni, walilala.

Mtoto punda akaota kuwa mamake alikuwa mgonjwa na alikuwa anamwita.

16

Alipoamka, mawingu yalikuwa yametoweka na mzee rafikiye alikuwa hayupo.

17

Hatimaye, mtoto punda alifahamu atakavyofanya.

18

Mtoto punda alirudi nyumbani akamkuta mamake amenuna.

Mama na mtoto wake mpotevu walitazamana kwa muda mrefu. Halafu wakakumbiatiana bila legezo.

19

Mtoto punda na mamake waliishi pamoja kwa ushirikiano.

Waliishi kwa furaha pamoja na majirani wao.

20
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Mtoto Punda
Author - Lindiwe Matshikiza
Translation - Translators without Borders
Illustration - Meghan Judge
Language - Kiswahili
Level - First paragraphs