Siku niliyokwenda Jijini
Lesley Koyi
Brian Wambi

Kituo cha basi cha kijiji chetu kilikuwa na shughuli nyingi. Basi zilijaza mizigo huku abiria wakizitafuta basi walizotaka kuabiri.

Kondakta waliwaelekeza abiria kwenye basi zilizokwenda sehemu mbalimbali.

1

Nilimsikia kondakta mmoja akiita kwa sauti, "Jiji! Jiji! Wanaokwenda magharibi!" 

Lile ndilo basi nililohitaji kuabiri kwa usafiri wangu.

2

Basi la kwenda jijini lilikuwa karibu kujaa. Hata hivyo, watu zaidi walitaka kuingia.

Baadhi yao walipakia mizigo chini ya basi. Wengine waliiweka ndani kwenye rafu.

3

Baadhi ya abiria walishika tiketi zao huku wakitafuta viti vilivyokuwa wazi.

Wanawake waliokuwa na watoto wachanga waliwatayarisha kwa safari hiyo itakayokuwa ndefu.

4

Nilipenyeza ndani nikapata kiti karibu na dirisha.

Abiria aliyeketi karibu nami alishika karatasi ya plastiki ya kijani kibichi. Alivaa viatu vilivyozeeka na koti kukuu.

5

Nilitazama nje nikawaza, "Ninaondoka hapa mahali nilipolelewa nikienda kwenye jiji kubwa. Sijui ikiwa nitawahi kurudi hapa kijijini tena."

6

Upakiaji mizigo ulikamilika na abiria wakawa wameketi.

Wachuuzi walizidi kusukumana wakitaka kuuza bidhaa zao. Walitaja majina ya bidhaa walizouza kwa sauti ya juu. Maneno yao yalinifurahisha.

7

Baadhi ya abiria walinunua vinywaji. Wengine walinunua vitavunaji vidogo na kutavuna.

Wasiokuwa na hela, kama mimi, walitazama tu.

8

Shughuli hizo zilikatizwa kwa mlio wa honi ya basi. Tulikuwa tayari kuondoka.

Kondakta aliwataka wachuuzi wote washuke kutoka basini.

9

Wachuuzi walisukumana kutoka nje. Wachache waliwarudisha abiria masalio ya hela zao.

Wengine walifanya juhudi za mwisho kuuza bidhaa zao.

10

Basi lilipoondoka kituoni, nilichungulia dirishani.

Nilikitazama kituo hicho kilichojaa magari nikiwaza, "Pengine hii itakuwa mara yangu ya mwisho kukiona kituo hiki."

11

Safari ilipoendelea, nilihisi joto jingi.

Niliyafumba macho nikinuia kulala.

12

Nilijiuliza maswali mengi. "Je, mamangu atakuwa salama? Je, sungura wangu watatufaidi? Je, ndugu yangu atakumbuka kunyunyizia maji miche ya miti yangu?"

13

Njiani, nilikariri jina la mahali mjombangu aliishi kule jijini.

Hatimaye, nilipatwa na usingizi.

14

Baada ya saa tisa, niliamshwa kwa kelele nyingi. Kondakta alikuwa akiwaita abiria waliotaka kwenda kijijini kwetu.

Nilichukua mkoba wangu mdogo nikaruka nje.

15

Basi hilo lililokuwa likirudi lilikuwa linajaa upesi. Muda mfupi baadaye, lingeanza safari ya kwenda mashariki.

La mhimu kwangu, lilikuwa kuanza kutafuta nyumba ya mjombangu.

16
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Siku niliyokwenda Jijini
Author - Lesley Koyi, Ursula Nafula
Translation - Ursula Nafula
Illustration - Brian Wambi
Language - Kiswahili
Level - First paragraphs