Magozwe
Lesley Koyi
Magriet Brink

Katika jiji moja, kuliishi wavulana wa kurandaranda mtaani. Asubuhi moja walikuwa wakikoka moto kutumia karatasi walizookota.

Miongoni mwao alikuwepo Magozwe, aliyekuwa mdogo kuliko wote.

1

Wazazi wa Magozwe walifariki akiwa na umri wa miaka mitano tu. 

Magozwe alienda kuishi na mjombake ambaye hakumjali. Alifanya kazi nzito bila kupewa chakula.

2

Magozwe alipolalamika, mjombake alimpiga. Alipotaka kwenda shule, mjombake alisema, "Usinisumbue. Wewe ni mjinga. Hata huwezi kujifunza chochote."

Baada ya kuteswa kwa miaka mitatu, Magozwe alitoroka akaanza kuishi mtaani.

3

Maisha ya mtaani yalikuwa magumu. Walikosa chakula. Walikamatwa na polisi. Walichapwa na wananchi na pia walikuwa wagonjwa.

Mara kwa mara, kulikuwa na vita baina yao na makundi mengine. Wavulana hao walitegemea kuombaomba. Pia waliuza plastiki, vyuma, chupa na magazeti makuukuu.

4

Siku moja, Magozwe aliokota kitabu cha hadithi. Alikikukuta vumbi na kukiweka ndani ya gunia lake.

Kisha alizitazama picha kwani hakujua kusoma maneno.

5

Kitabu kilikuwa na picha za mvulana aliyekuwa rubani wa ndege. Magozwe alitamani sana kuwa rubani. Ndoto yake ilikuwa awe rubani bora zaidi ulimwenguni.

Mara nyingi aliyafumba macho na kuwaza kuwa alikuwa akiendesha ndege kubwa kuliko zote!

6

Ulikuwa msimu wa baridi. Magozwe aliombaomba barabarani. Mwanamume mmoja alimsalimu na kujitambulisha kwake, "Hujambo? Ninaitwa Tomaso. Ninapajua mahali unapoweza kupata chakula."

Tomaso alimwonyesha nyumba yenye paa la bluu. Magozwe alimtazama Tomaso, akaitazama ile nyumba kisha akasema, "Labda." Akaondoka na kwenda zake.

7

Miezi iliyofuata, wavulana wa mtaani walikuwa wamezoea kumwona Tomaso. Tomaso alipenda kuzungumza na watu walioishi mtaani. Aliwasikiliza wakizungumzia maisha yao. 

Tomaso alikuwa na nia nzuri, mvumilivu na mwenye heshima. Baadhi ya wavulana walianza kwenda katika nyumba ya paa la bluu. Wakati wa mchana walipata supu na mkate.

8

Magozwe alipokuwa akikitazama kitabu alichokiokota, Tomaso alimwuliza, "Hadithi hiyo inahusu nini?" 

Magozwe alimjibu, "Nadhani inamhusu mvulana aliyekuwa rubani."

"Anaitwaje?" Tomaso alimwuliza. Magozwe alijibu kwa sauti ya chini, "Sijui. Siwezi kusoma."

9

Baadaye, Magozwe alimweleza Tomaso sababu iliyomfanya atoroke kwa mjombake. Tomaso alimsikiliza ila hakumfanyia uamuzi.

10

Magozwe aliposherehekea miaka kumi ya kuzaliwa kwake, Tomaso alimpatia kitabu kipya cha hadithi. Kilimhusu mvulana mchezaji kandanda maarufu.

Tomaso alimsomea Magozwe hadithi hiyo kila mara. Siku moja alisema, "Wakati wa kwenda shule umefika. Utaweza kujisomea. Unaonaje?"

Tomaso alimwonyesa mahali watoto waliposaidiwa kwenda shule.

11

Magozwe alianza kufikiria kuhusu mahali hapo na kuhusu kwenda shule.

"Labda mjombangu alisema ukweli kwamba mimi ni mjinga na siwezi kujifunza chochote? Na je, nikipigwa huko nitafanyaje? Labda ni heri kubaki mtaani."

Magozwe aliyafikiria mambo hayo kwa hofu.

12

Magozwe alimwelezea Tomaso mawazo yake na hofu aliyokuwa nayo.

Muda ulipopita, Tomaso alimshawishi Magozwe. Alimwambia kuwa maisha yake yangekuwa bora iwapo ataenda shule.

13

Magozwe alihamia katika chumba kimoja kwenye jumba kubwa. Alikitumia chumba hicho pamoja na wavulana wengine wawili. Jumla, walikuwepo watoto kumi walioishi katika jumba lile.

Waliishi na Shangazi Cissy na mumewe, mbwa watatu, paka na mbuzi mmoja.

14

Magozwe alipoanza kwenda shule, haikuwa rahisi. Mara nyingi alitaka kukata tamaa.

Lakini, alipokumbuka rubani na mchezaji kandanda maarfu aliowasoma katika vitabu vya hadithi, alivumilia.

15

Siku moja Magozwe alipokuwa akisoma kitabu, Tomaso alimwuliza, "Hadithi unayoisoma inahusu nini?"

Magozwe alimjibu, "Inamhusu mvulana aliyekuwa mwalimu." "Anaitwaje?" Tomaso alimwuliza tena.

"Anaitwa Magozwe." Magozwe alisema kwa tabasamu.

16
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Magozwe
Author - Lesley Koyi
Translation - Ursula Nafula
Illustration - Magriet Brink, Wiehan de Jager
Language - Kiswahili
Level - Read aloud